BIASHARA UTOTONI NA ELIMU
Mtoto Samson Hezron (11) mwanafunzi wa darasa la nne katika shule ya Msingi Ngh'ongh'onha katika Manispaa ya Dodoma ni miongoni mwa wanafunzi wa shule za msingi wanao juihusisha na biashara wakiwa na lengo la kusaidia kuinua kipato cha familia zao.
Samson akionge na MED alisema kuwa anafanya biashara ya miwa ili kuongeza kipato kwenye familia na kuweza kupata fedha za kukidhi mahitaji yake muhimu yakiwemo ya sare na madaftari ya shule.
"Baba na mama yangu hawana kazi japo baba amesoma hadi darasa la saba; nikipata fedha nampa mama kwa ajili ya chakula na nyingine naweka kwa ajili ya mahitaji ya shule"
Samson anadai kuwa hufanya biashara kwa kufuata ratiba ya nyumbani kuwa ni lazima awe nyumbani kabla ya saa kumi na moja jioni wakati hufanya biashara kwa siku za jumamosi, jumapili, siku za mapumziko na likizo.
Kijana huyu anaongeza kuwa pamoja na kufanya biashara katika umri mdogo ratiba yake ya masomo anaiheshimu na kujikuta akipata si chini ya alama 70 kwa somo la Hisabati, 80 kwa sayansi na 30 kwa somo la kiingereza. "Kiingereza ni kigumu sana kwangu; hata hivyo mwalimu wa kiingereza na sayansi Mwl. Luganissa nampenda sana kwani anaelekeza vizuri bila viboko"
Kijana Samson akiwa na miwa yake tayari kuelekea mitaani kutafuta waeja wa miwa.
Mtoto Samson nadai kuwa mtaji wake wa miwa ni kiasi cha sh 2000 ambazo humpatia faida ya kati ya sh 2000 hadi 2500 kwa siku. Kuhusu kupata muda wa kujisomea "Sam" anasema hasomi tuition kwani kaka yake anayesoma darasa la saba ana mfundisha kila siku kuanzia saa 12 jioni nyumbani kwao.
Kijana Samsoni ni mmoja kati ya watoto wanaofanya biashara mbalimbali mkoani Dodoma kwa lengo la kukabiliana na hali ngumu ya maisha katika gfamilia zao. Wengi wa vijana wenye umri sawa na wa Samson hujihusisha na kuomba-omba mitaani, biashara ya vyuma chakavu na kuokota chupa za plastiki na kuziuza kwa wafanya biashara wa chupa hizo.
KIKUYU YAUNDA KAMATI YA KURATIBU SHUGHULI ZA CLUB ZA MARAFIKI
Marafiki wa Elimu katika shule ya Sekondatri Kikuyu wameamua kuunda kamati ya shule kwa ajili ya kuratibu shughuli za Marafiki ili kuongeza ufanisi na uendelevu wa harakati za Marafiki katika shule hiyo. |
Uamuzi wa wanaharakati hao kuwa na Kamati hii ni kuhakikisha kuwa Marafiki wa shule hiyo wanafanya kazi yao kwa umakini zaidi na kuongeza tija katika mijadala na uhuru wa kutoa maoni na kuchangia mada mbalimbali za Club za Marafiki katika shule hiyo.
Shule ya Kikuyu ina jumla ya Club 9 za Marafiki ambazo zinahusisha mikondo 9 ya kidato cha kwanza hadi cha tatu. “Kuundwa kwa Kamati hii kutasaidia kuimarisha uhuru wa mijadala na kuzifanya Club zidumu kwani zitasimamiwa na wanafunzi wenyewe”. Club za Marafiki wa Elimu Kikuyu zinajiendeshwa kwa kusimamiwa na Kamati ya Marafiki wa Elimu Dodoma kwa kushirikiana na Mwalimu Mlezi wa Club hizo.
Timu ya Marafiki wa Elimu katika shule ya Sekondari Kikuyu Mkoani Dodoma imeonesha mabadiliko makubwa katika kutetea walimu kwa kutoa wito kwa wadau mbalimbali kuwatetea walimu ili kupata stahiki zao na kuboresha ari ya walimu kufanya kazi zao pasipo kinyongo.
Wanaharakati hao wameeleza kuwa kuendelea kushuka kwa kiwango cha ufaulu katika shule za sekondari hasa za kata ni matokeo ya kupuuzwa kwa ushauri wa walimu au walimu kusahaulika. Vijana hao wamewataka wadau hasa taasisi na mashirika yasiyo ya kiserikali kusaidia kupaza sauti juu ya kilio cha walimu ili kuwaongezea ari katika kutekeleza majukumu yao.
MARAFIKI WAJADILI NAMNA YA KUBORESHA MMES II- MOROGORO
Wawakilishi wa harakati za Marafiki wa Elimu kutoka kanda tatu za Mashariki, Kusini na Nyanda za juu Kusini; walikutana mjini Morogoro kwa ajili ya kujadili masuala mbalimbali yanayohusu mustakabali wa Elimu na namna nzuri ya kuboresha ushiriki wa wananchi katika utekelezaji wa mipango ya maendeleo ya Elimu.
Aidha washiriki hao waliipongeza Serikali kwa juhudi zake za kuboresha kiwango cha Elimu kupitia mipango yake ya maendeleo ya Elimu kama MMEM I&II, MMES I&II na Mafunzo ya Ualimu Kazini (TDMS).
Wanaharakati hao walitambua mafanikio ya mipango hiyo kuwa ni pamoja na kufanikiwa kujenga shule nyingi za msingi na sekondari, ongezeko kubwa la uandikishaji wa watoto katika shule zetu, ongezeko la juhudi za kupeleka pesa shuleni kwa lengo la kuboresha hali ya vifaa vya kufundishia na kujifunzia katika shule nyingi hapa nchini. Moja ya Maktaba katika Shule ya Sekondari zilizoko Mkoani Dodoma.
Ushauri ulitolewa na wanaharakati hao kwa serikali kwamba; katika kutekeleza MMES II uliozinduliwa Januari 2011; ambao unalenga kuboresha kiwango cha elimu ya sekondari, uandikishaji wa wanafunzi, mfumo wa uongozi na mfumo wa ukaguzi; ni budi serikali iyafanyie kazi mapungufu yaliyojitokeza kwenye mipango iliyopita.
Walitaja mapungufu yaliyojitokeza katika mipango iliyopita kuwa ni pamoja na udahili wa wanafunzi shuleni ambapo wanafunzi wenye hata chini ya alama 150 walichaguliwa kujiunga na elimu ya sekondari, watendaji wa mipango hiyo hasa wakuu wa shule, bodi na kamati za shule kutokuwa na elimu ya kutosha kuhusiana na mipango na kwa kiasi kikubwa wananchi ambao ndio wadau wakuu hawakuelimishwa wala kushirikishwa kama mpango unavyoeleza.Wanafunzi wa darasa la Saba wanaojiandaa kuingia kidato cha kwanza 2012.
Marafki wa Elimu kwa kauli moja waliazimia kuishauri serikali kutekeleza mambo 6 ambayo wanaamini kuwa kama yatafanyiwa kazi ipasavyo; mafanikio chanya yatapatikana katika maendeleo ya elimu haa nchini. Maazimio hayo ni pamoja na:-
- Serikali ihakikishe kuwa inapeleka fedha za ruzuku mashuleni kwa kiwango cha mpango kwa wakati.
- Serikali ihakikishe kuwa wadau wote muhimu katika kutekeleza mpangio wanakuwa na uelewa wa kutosha kwa kuelimishwa kuhusu wajibu wao, haki zao na kushirikishwa kikamilifu katika kila hatua yautekelezaji.
- Serikali ihakikishe kuwa inaimarisha ukaguzi wa ndani na wa nje katika shule na pia ukaguzi huo ufanyike mara kwa mara ili kudhibiti na kubaini ubadhirifu wa rasilimali za shule.
- Serikali izingatie viwango vya ufaulu vilivyotamkwa kwenye serra ya Elimu katika kuchagua watoto wa kujiunga na elimu ya sekondari na kuhakikisha kuwa taarifa za maendeleo ya wanafunzi pamoja na matokeo halisi ya mwisho yanakuwa ndio kigezo cha kumchagua mwanafunzi kujiunga na sekondari.
- Serikali ihakikishe kuwa inaongeza idadi ya walimu mashuleni na kuwapatia walimu mafunzo kazini mara kwa mara na kuboresha mazingira ya walimu hasa wanaofanya kazi maeneo ya vijijini.
- Serikali ihakikishe kuwa uteuzi wa wasimamizi wa shule unazingatia vigezo vya uteuzi kama miongozo inavyoelekeza; wakuu wa shule wapewe semina za mara kwa mara kwa ajili ya kuboresha utekelezaji wa majukumu yao na kuhakikisha kuwa Bodi na Kamati za shule zinajengewa uwezo wa mara kwa mara ili kuboresha usimamizi wa majukumu yao.
Tamko hili la wanaharakati halina budi kuungwa mkono na wadau wote wapenda maendeleo ya Elimu nchini hasa kwa kuzingatia ushindani wa ubora wa Elimu tunaokabiliana nao hasa katika Muungano wetu wa Jumuia ya Shirikisho la Afrika Mashariki.
SHULE TUNAZO; VITENDEAKAZI JE?
Wakati serikali yetu ikijinadi kuwa imepata mafanikio makubwa katika kuwezesha watoto wengi kujiunga na elimu ya msingi hapa nchini; bado kuna umuhimu mkubwa wa serikali kutafakari kwa kina kile watoto hawa wanachokipata katika shuleni hizo.
Ni ukweli usiopingika kwamba shule zetu za msingi zimepata wanafunzi wengi ambao kwa hakika wamejiunga na shule za msingi kwa ajili ya kupata elimu hii muhimu kwa maisha yao ya kila siku. Kwa hili tunapaswa kuipongeza serikali kwani wapo vijana wengi ambao kwa juhudi za serikali hasa kuiptia mpango wa MMEM wangeikosa fursa hii.
Pamoja na pongezi hizi; yapo mambo ambayo tunapaswa kuyatazama kwa mapana zaidi hasa katika suala zima la upatikanaji wa vitendea kazi kama vitabu vya kiada na ziada, walimu wa kutosha kwa masomo yote, madawati, vyumba vya madarasa, matundiu ya vyoo, mazingira safi nya kujifunzia na kufundishia na viwanja vya michezo kwa watoto wetu.
Ukosefu wa mahitaji muhimu au vitendea kazi hivyo na kutokuwepo kwa juhudi za dhati za kutatua tatizo hilo ni sawa na kuididimiza elimu na kuwapotezea muda vijana hawa ambao kila kukicha wanaitafuta elimu na kujikuta ndoto zao zikiishia hewani.
Kwa kitabu kama hiki anachokisoma kijana huyu aliyefahamika kwa jina moja la Issa mwanafunzi wa darasa la nne katika shule ya msingi Pahi Wilayani Kondoa; ni ushahidi tosha kuwa bado kijana huyu na wengine wengi wana safari ndefu ya kutimiza ndoto zao za kupata Elimu bora na yenye manufaa kwa maisha ya baadaye.
Wadau wote wa Elimu nchini; hatuna budi kumpongeza kijana huyu kwani licha ya kitabu hiki kubaki kipande baada ya kuliwa na wadudu ambao haijafahamika kama ni jamii ya mchwa au panya; bado ameendelea kuhitaji japo masalio ya kile kilichoandikwa kwenye kitabu hiki. Hongera sana Issa!
WILAYA YA KONDOA NA VITUKO KATIKA ELIMU
Halmashauri ya Wilaya ya Kondoa iliyoko umbali wa kilometa 160 kutoka Dodoma inakabiliwa na hali mbaya ya maendeleo ya Elimu kufuatia shule zake za Sekondari kudorora katika matokeo ya mitihani ya kitaifa ukiwemo wa kidato cha nne uliofanyika mwishoni mwa 2010. Kibao hiki kinaelekeza lugha rasmi ya kutumia kwenye shule ya Sekondari Changaa.
Kufuatia matokeo ya mtihani wa kidato cha nne yaliyo tangazwa na Baraza la Mitihani la Taifa mwanzoni mwa mwaka 2011; shule tano kati ya kumi zilizofanya vibaya kitaifa zilitoka katika Wilaya ya Kondoa ambazo ni Changaa, Kolo, Hurui, Kikore na Thawi.
Hii ni hali halisi ilivyo katika chumba cha darasa kinachotumika kama ofisi ya walimu.
Timu ya wanaharakati wa Elimu kutoka Asasi aya Marafiki wa Elimu Dodoma MED ilifanya ziara katika shule ya Changaa ambapo ilifanikiwa kufika kwa tabu kutokana na muiundombinu mibaya hasa ya barabara za kufika katika shule hiyo ambayo pia haina hata kibao cha kuelekeza jinsi ya kuifikia shule hiyo.
Ziara ya Marafiki wa Elimu Dodoma ilibaini vituko vya aina yake katika shule hiyo yenye wanafunzi wa kidato cha kwanza hadi cha nne na kuwaacha hoi kwa mshangao baada ya kubaini kuwa shule ya Changaa ina wanafunzi watatu (3) tu wa kidato cha nne kwa mwaka 2011 ambapo kati yao wasichana ni wawili na mvulana mmoja tu. Kurwa Martin mwafunzi pekee wa kidato cha nne kati ya watatu aliye hudhuria masomo wakati wa zira ya Marafiki wa Elimu katika shule ya Sekondari Changaa.
Sababu za uwepo wa wanafunzi watatu wa kidato hicho ilielezwa ni kutokana na wengi wao kukata tamaa ya matokeo mabaya na pia umbali wa kutoka shuleni na makazi ya wenyeji.
Wanafunzi wa shule hii tangu wajiunge na Elimu ya Sekondari hawajawahi kujifunza masomo ya Sayansi na Hisabati kutokana na kukosekana kwa mwalimu wa masomo hayo japo Mkuu wa shule hiyo ni walimu wa masomo hayo. Hii ni picha ya Maabara ya shule ya Sekondari Changaa iliyoko Wilayani Kondoa.
Imeelezwa kuwa 2009 shule hiyo ilikuwa na mwalimu mmoja; 2010 walimu wawili na 2011 shule ina walimu watatu wa kuajiriwa na mmoja wa kujitolea na kulipwa posho na jamii.
Wanafunzi wa Changaa wanatembea kwa zaidi ya kilomita sita kwa siku kwenda na kurudi shuleni kutokana na shule hiyo kuwa mbali na makazi ya watu jambo ambalo linachangia kwa kiasi kikubwa wengi wa wanafunzi hao kukosa hamu ya kuendelea na masomo.Wanafunzi wa Changaa Sekondari wakizitafuta Km3 za kurejea nyumbani.
Hakuna Maisha Bora Bali Bora Maisha.
Familia moja katika Kata ya Kikuyu Kusini Manispaa ya Dodoma itaubaliana na kauli yangu kwa Bora Maisha kwa Kila Mtanzania na ukweli si Maisha Bora kwa kila Mtanzania kama ambavyo kauli hiyo imekuwa ikiimbwa kila kukicha na viongozi wetu wa Serikali na hata wa hama Tawala CCM.
Kwa zaidi ya mwezi mmoja na nusu sasa moja kati ya nyumba zilizoathiriwa na mvua zilizonyesha mjini Dodoma tangu mwishoni mwa mwezi Januari haijafanyiwa ukarabati licha yafamilia hiyo kuendelea kuitumia nyumba hiyo huku kila siku wakizidisha sala na kujikabidhi mikononi mwa muumba kwa lolote linaloweza kutokea.
Unadhani familia hii itachagua lipi kati ya Maisha Bora kwa Kila Mtanzania na Bora Maisha kwa Kila Mtanzania? Ni wazi kwamba jibu la familia hii unalo. Tuachane na nyumba ya mpiga kura huyu na kuangalia suala la usafi wa mazingira na hasa suala la choo; KARIBU!
Hiki ndicho choo kinacho tumiwa na familia hii; hiki ni kipindi cha mvua ambacho kwa kawaida kipindupindu nacho hushika hatamu. Bado najiuliza juu ya Familia hii; inaihesabu na kuikubali SERIKALI NA KAULI ZAKE? Majibu na ushauri wako ni muimu sana!
Wanaharakati Wajadili Mchakato wa Katiba Mpya.
Mchakato wa kuandika katiba mpya ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania unazidi kushika kasi zaidi nchini baada ya wanaharakati wa mikoa saba kukutana Dodoma kujadili na kujifunza juu ya katiba ya sasa na mapungufu yake na jinsi ya kuelimisha wananchi umuhimu wa kuwa na katiba mpya.
Warsha hiyo ya sikun tatu inafanyika katika Hoteli ya Dodoma inahudhuriwa na wawakilishi wa Mitandao ya Asasi za Kiraia kutoka katika Mikoa ya Morogoro, Lindi, Rukwa, Ruvuma, Iringa, Mbeya Dodoma na Tabora.
Washiriki wa warsha hiyo wameeleza nia yao ya kuhakikisha kuwa watadumu katika kuulinda Muungano wa Tanganyika na Zanziba na kuahidi kuwa watajitahidi kuhakikisha katika mchakato huo watajitahidi kuziondoa kasoro zinazoonekana kuwa zinayumbisha Mungano huo.
Wakichangia mada katika warsha hiyo inayoonekana kuwavuta wanaharakati ha ambao ni waumini wa Asasi za kiraia nchini wamesema kuwa kazi ya kuelimisha jamii juu ya uwepo wa Katiba Mpya ni ya muhimu inayohitaji kujituma na kuwa na moyo wa kujitolea kuisaidia jamii ili ielimke na kuwa na maamuzi yaliyo sahihi na yenye manufaa kwa Taifa.
Naye Mkufunzi wa warsha hiyo Bw. Deus Kibamba (picha ndogo)kutoka Jukwaa la Katiba amesema watanzania watashiriki kwa mara ya kwanza kutunga katiba yao kwani katiba iliyopo kwa sasa hakutungwa na watanzania bali watanzania waliletewa katiba hiyo iliyotungwa na waingereza.
Washiriki wa warsha hiyo wamempongeza Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mh. Dk. Jakaya Mrisho Kikwete kwa kukata kiu ya watanzania katika kudai katiba mpya.
Wadau hao walisema kuwa kauli ya Rais aliyoitoa kwenye maadhimisho ya sherehe za kutimiza miaka 34 ya kuzaliwa kwa CCM mkoani Dodoma tarehe 5 Februari, 2011 ilimaliza utata uliokuwepo kutokana na kauli tata za baadhi ya watendaji wake kama Mwanacsheria Muu wa Serikali na Waziri wa Sheria na Katiba.
Warsha hiyo inayoendeshwa kwa mtindo shirikishi kwalengo la kuwafanya washiriki wote wajisikie kuwa sehemu ya mchakato huo; imekuwa ya mafanikio makubwa hasa kutokana na wengi wa washiriki kuonekana kuwa makini na wasikivu katika kila hatua.
Tanzania, Tanzania; nakupenda kwa moyo wote.... Wanaharakati waliimba wimbo huo kuonyesha mshikamano wao kwa Tanzania na nia yao njema ya kudumisha Muungano huo ambao wamesema ni wa kipekee duniani hivyo hauna budi kuendelea kuwepo ili kuiweka Tanzania katika historia hiyo.
Kwani Viongozi wetu Hawaoni?
Wananchi wa Kata ya Hazina iliko shule ya Msingi wanajiuliza swali mkwamba "Kwani viongozi wetu hawaoni?" wakazi hawa wamefikia hatua hiyo mara baada ya kutosikia hatua zozote zilizochukuliwa na ama viongozi wa Mkoa, Wilaya, au Tarafa kuhusiana na vyumba viwili vya madarasa vilivyojengwa katika shule hiyo kuharibika vibaya kutokana na kujengwa chini ya kiwango.
Jengo hili lililojengwa kwa fedha za MMEM II; halifaimkwa shughuli zozote kutokana na kuwa a nyufa zinazotihia kila aina ya kiumbe hai kinachothamini uhai wake.
Hapa ndipo tunapojiuliza kama kweli rasilimali za umma zinatumika ipasavyo au la; jamii nayo inapaswa kuwajibika katika kusimamia vyema rasilimali za umma badala ya kuiachia serikali ambayo kazi hizi mbovu zinapofanyika viongozi wanakuwa hawahusiki.
Kero ya Maji Kikuyu Hadi lini?
Wakazi wa kata ya Kikuyu Kusini Manispaa ya Dodoma hawajui hatima yao dhidi ya kero ya maji wanayo endelea kuipata kwa miongo kadhaa hadi sasa. wakazi hao wamekuwa wakitumia maji ya visma vifupi yasiyo safi wala salama kwa kipindi kirefu imeelezwa.
Kama picha inavyoonesha hapo juu; wakazi hawa wamedai kuwa wameishi katika kata ya Kikuyu kwa zaidi ya miaka ishirini na matumaini pekee waliyo nayo kuhusiana na maji ni visima vifupi wanavyo vitumia katika eneo hilo lenye wakazi wa kipato cha kati.
Licha ya kukubali kupigwa picha na kukataa kutaja majinayao; wakazi hao wameeleza kuwa wamedumu kwenye eneo hilo tangu enzi za diwani mkongwe wa eneo hilo Al-maarufu Mkungugu Marehemu Mloge aliyedumu kwenye udiwani wa eneo hilo kwa awamu nne; Meya mstaafu wa Manispaa ya Dodoma na Diwani wa eneo hilo Mh Francis Mazanda na baadaye Kata hiyo ilimpata Diwani ambaye walimtaja kwa jina la Baba Jofu ambaye alichaguliwa katika uchaguzi wa 2010 lakini alifariki dunia kabla ya kuapishwa.
Wakazi hao wamedai kuwa eneo hilo limesahaulika kwa kipindi kirefu kwa huduma hiyo muhimu licha ya ahadi kede-kede zinazotolewa na viongozi mbalimbali wa kisiasa na serikali kila wakati kuwa watatatua kero hiyo.
Wakazi hao wameeleza kuwa maji hayo yanayo patikana kwenye visima vifupi vilivyopo kando ya barbara ya Iringa hatua chache kutoka stendi ya daladala za Kikuyu si safi wala salama kwa matumizi ya binadamu.
Eneo la Kikuyu ni miongoni mwa maeneo yenye uhaba mkubwa wa huduma ya maji safi na salama jambo ambalo linasababisha usumbufu mkubwa kwa wakazi wa eneo hilo kwa kulazimika kutumia muda mrefu kutafuta maji.
Wazazi waaswa na Tuisheni za wanavyuo.
Wazazi wa wanafunzi wanaosoma katika shule ya Sekondari ya Kikuyu Manispaa ya Dodoma wameaswa kujihadhari na Tuisheni zinazoendeshwa na wanavyo kwani zina madhara makubwa kuliko faida.
Rai hiyo ilitolewa kwenye mkutano wa wazazi wa wanafunzi wa kidato cha pili na cha nne wanaosoma katoka shule hiyo kufuatia malalamiko kuwa wengi wa wanafunzi wa shule hiyo wanajihusisha na masuala ya ngono na wanachuo wa St. Johns.
Wazazi na walimu wa shule ya sekondari ya Kikuyu walieleza masikitiko yao mbele ya Mwenyekiti wa Kamati ya maendeleo ya Kata ya Kikuyu Kaskazini Mh. Meja Risasi kuwa, baadhi ya wanafunzi wa kike katika shule hiyo wamekuwa wakisingizia kufundishwa na wanachuo hao lakini matokeo yake wanaishia kufanya nao ngono badala ya masomo.
Wazazi hao wameombwa kuhakikisha kuwa wanawalinda watoto wao dhidi ya mtego wa wanachuo kwa kuhakikisha kuwa wanawazuia kwenda kwenye tuisheni hizo bandia.
Ili kupunguza tatizo hilo; Mkuu wa shule ya Kikuyu Sekondari Bi. Mkoyi aliwaeleza wazai kuwa shule hiyo imeazimia kuwa wanafunzi wa kidato cha pili na tatu watafanya marudio ya masomo kila siku za masomo bila malipo hivyo wazazi wahakikishe kuwa wanawawezesha watoto wao angalau kwa fedha ya kujinunulia soda mchana ili wasirudi nyumbani mara baada ya masomo ya kawaida.
Wazazi waliupongeza walimu na uongozi wa shule hiyo ambayo katika matokeo ya kidato cha nne 2010 zaidi ya wanafuzi 40 walifaulu katika daraja la kwanza hadi la tatu.