Envaya
Parts of this page are in Swahili. Edit translations

large.jpg

Wanafunzi wa shule ya msingi Nghaheleze iliyoko Wilayani Chamwino wakiwa kwenye picha ya pamoja baada ya kupokea msaada wa Vitabu vya kiada. Vitabu hivyo vilikabidhiwa kwao na shirika la Marafiki wa Elimu Dodoma.

large.jpg

Mkuu wa Wilaya ya Chamwino Mkoani Dodoma Bi. Fatma Said Ally akiongea na wadau wa Elimu wakati wa uzinduzi wa mradi wa My Rights My Voice unaotekelezwa na Asasi ya Marafiki wa Elimu Dodoma (MED) na Women Wake UP (WOWAP) kwa uhisani wa Shirika la Oxfam GB. Pichani mwenye shati la Blue ni Mratibu wa MED Bw. Davis Makundi na mwenye shati la Black ni Kaimu Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya ya Chamwino BBaltazary Ngowi.

                                      HAKIELIMU YAPONGEZWA                           Na. Davis Makundi

Shirika la HakiElimu limepongezwa kwa kazi nzuri wanayoifanya nchini hasa katika kuboresha  Elimu na Demokrasia nchini. Pongezi hizo zimetolewa na Mwenyekiti wa Bodi ya Asasi ya Marafiki wa Elimu Dodoma (MED) Dk. Sinda Hussein Sinda ambaye pia ni Mhadhiri wa Chuo Kikuu cha Dodoma UDOM wakati akifungua mkutano wa wajumbe wa Bodi hiyo ambayo ni ya kwanza tangu MED kupata usajili rasmi.

Dk. Sinda pichani alisema mara nyingi mashirika yanayofanya kazi na wadau wake hupenda kuwatumia wadau hao kama chambo cha kuwapatia umaarufu kwa ajili ya kujikuza wao lakini kwa HakiElimu imekuwa tofauti kwani hadi hatua za mwisho wa usajili waliendelea kutoa ushirikiano kwa MED hadi usajili ukapatikana. "Ndugu wajumbe, tuna kila sababu ya kuwashukuru HakiElimu kwa jambo hili ambalo sote tunaamini bila wao leo hii MED isingekuwepo" alisema Dk. Sinda.

Naye Mratibu wa MED Bw. Davis Makundi aliwaeleza wajumbe kuwa ushirikiano huo umezidi kuimarika kwani HakiElimu licha ya kukubali jina la "Harakati za Marafiki wa Elimu" litoholewe na MED na kutumika; mwishoni mwa mwezi Aprili, 2012 walituma mkataba wa sh. 1,370,000/= kwake kwa ajili ya kuendesha vipindi 10 vya radio Mkoani Dodoma vitakavyohusiana na Elimu, Demokrasia na masuala ya utawala Bora.

Bodi ya MED inaandaa utaratibu wa kufanya mawasiliano na HakiElimu kwa ajili ya kuwaomba wakubali kuwa wanachama wa heshma katika shirika la MED kwa mujibu wa katiba.

Wakati huo huo wananchi wa kijiji cha Chidachi kilichoko Kata ya Mkonze Manispaa ya Dodoma wamesema wanatamani sana HakiELimu ikubali kuwa Mlezi wa Shule ya Msingi Chidachi ambayo licha ya kuwa ni shule changa, imekuwa na mafankio makubwa kitaaluma siku hadi siku.

Mwalimu Mkuu wa Shule hiyo Bi. Zuhura Muhoji pichani kulia; alitoa ombi hilo kwa asasi ya MED na kuiomba iwasiliane na HakiElimu katika kufuatilia suala hilo. Wazazi na wanajamii wa Mkonze walieleza kuwa HakiElimu limekuwa ni shirika lisilo la kiserikali lenye mfano wa kuigwa kutokana na shughuli zake kuigusa jamii moja kwa moja tofauti na mashirika mengine ambayo yamekuwa yakifanya kazi kwa hisia za mahitaji ya jamii badala ya kuangalia hali halisi ya matatizo ya jamii husika. Shule ya Chidachi ilianzishwa katika Mpango wa MMEM na kuanza kupokea wanafunzi mwaka 2004. Mahafali ya kwanza ya shule hityo yalifanyika 2006 ambapo ufaulu ulikuwa 100%. Mahafali zilizofuata matokeo yake ni kama yanavyoonekana kwenye mabano; 2007 (91%) 2008 (88.8%) 2009 (86.9%) 2010 (87.5%) na 2011 (100%). Pamoja na mafanikio hayo kwa shule ya Chidachi, shule ina upungufu mkubwa wa madawati, nyumba za Walimu, vitabu vya kiada na ziada pamoja na changamoto ya Maktaba.

CLUB ZAOMBA MAKTABA, TUISHENI KUNUSURU UFAULU KIDATO CHA  IV, 2012

Na. Davis Makundi

Wanachama wa Club za Marafiki wa Elimu Dodoma kutoka katika shule mbalimbali Mkoani Dodoma wameomba msaada wa kupata walimu na Maktaba za jamii ili kuwanusuru na matokeo mabaya katika mtihani wa kidato cha nne na kidato cha pili mwaka huu.

Wanachama hao ambao ni wanafunzi wa shule za sekondari kutoka katika shule mbalimbali ndani ya Manispaa ya Dodoma wamesema ili kuhakikisha kuwa wanachama wa Club hizo wanakuwa mfano wa kuigwa katika matokeo yao ni vyema uwepo mkakati wa aina yake wa kuongeza ufaulu kwa kuwapatia wanachama hao masomo ya ziada na fursa ya huduma za Maktaba ili kuongeza ufaulu wao.

Maombi hayo ya wana Club yamekuja kufuatia uchambuzi uliofanywa na wanachama hao kwa ushirikiano na MED kuhusu kero ambazo zinawafanya wasifanye vizuri kwenye mitihani yao ya kidato cha pili na ile ya kidato cha nne. 

Wakiongea katika mjadala huo wanafunzi hao wamekiri kuwa juhudi za ziada za kila mwanafunzi zinachangia kwa zaidi ya asilimia 70% kiwango cha 30% kilichosalia kinapaswa kutoka kwa walimu, jamii, wazazi na wadau wengine. "tunajitahidi lakini wadau wengine nao watusaidie kupata vitabu na walimu kwa masomo ya ziada ili tufaulu" alisema Charles Chunga pichani mwanafunzi wa kidato cha tatu katika shule ya Kikuyu Sekondari.

Wakiunga mkono wazo hilo wanafunzi hao walitoa ombi kwa wadau kuchangia uanzishwaji wa Maktaba za jamii na kutafuta namna ya kuwezesha walimu wa masomo ya ziada ili wanafunzi wasio na uwezo wa kujiunga na Maktaba ya Mkoa na malipo makubwa ya tuisheni wapate huduma hiyo kwa gharama nafuu au bure kabisa pale inapo wezekana. ___________________________________________________________________________

MVUA YAEZUA PAA, MABATI YAANIKWA KWENYE NYAYA ZA UMEME   Na. Baraka Mosi

Mvua iliyoambatana na upepo iliyonyesha juma lililopita imeezua paa la nyumba moja katika Mtaa wa Chidachi Kijiji cha Mkonze Manispaa ya Dodoma na kuiacha familia hiyo ikiwa haina mahali pa kuishi. 

Sehemu kubwa ya paa la nyumba hiyo lililoezuliwa lilisukumwa na upepo na kutua kwenye nyaya za umeme hali iliyo ufanya mtaa huo kukosa umeme kwa muda wa siku mbili mfululizo.

Taarifa zaidi zinasema kuwa hakunamtu aliyejeruhiwa kufuatia tukio hilo lililotokea usimu wa kuamkia jumamosi ya juma lililopita.

___________________________________________________________________________

ULE USEMI WA "MVUMILIVU HULA MBIVU" UMETIMIA          Na. Davis Makundi


Ni kama utani lakini ni kweli imetimia kwa binti Kurwa Martin Ng'ondi mwanafunzi wa kidato cha nne (iv) katika shule ya sekondari Changaa iliyoko katika Halmashauri ya Wilaya ya Kondoa Mkoani Dodoma. Katika shule hiyo iliyokuwa na wanafunzi watatu (3) wa kidato cha nne wakiwemo wasichana wawili na mvulana mmoja; ni Kurwa pekee aliyehudhuria masomo shuleni hapo mnamo tarehe 4 Aprili, 2011 tulipofanya ziara shuleni hapo.

Akizungumza kwa kujiamini na kuwa na uhakika wa alichikuwa akikisema, Kurwa alituahidi kuwa havunjwi moyo na idadi ndogo ya wanafunzi wa darasa lake na uhaba wa walimu katika shule hiyo bali yeye anacho hitaji ni kuhitimu masmo yake ya kidato cha nne. "najua kuwa nakabiliwa na changa moto ya uhaba wa walimu, idadi ndogo ya wanafunzi na uhaba wa vifaa hapa shuleni; lakini kwangu hili nitakabiliana nalo hadi nimalize masomo ya kidato cha nne" alisema Kurwa."

Ahadi ya binti huyu ilitimia baada ya kuvumilia na kuvuna mbivu zake kwa kufanya mtihani wa kidato cha nne na kuambulia alama 35 ambazo si nzuri kwa wahitimu wetu. Kwa Kurwa yeye angeepuka vipi alama hizi kama darasani wako watatu (wasichana wawili na mvulana mmoja) na shule yake yenye wanafunzi wa kidato cha kwanza hadi cha nne ina walimu watatu?

Kurwa Martin na Zainabu Idi wao walipata alama 35 wakati Yasini Ali yeye alipata alama 33 baada ya kupata daraja D katika masomo ya CIV na GEO. Uvumilivu wa vijana hawa na matokeo yao ni kichocheo kwa vijana wote walio katika shule zetu za kata kutambua kuwa licha ya changamoto ya walimu, vifaa, na mazingira magumu ya kujifunzia na kufundishia; wanapaswa kufanya juhudi za ziada ili kufikia malengo yao. ___________________________________________________________________________

SHULE YAFAULISHA 100%; YAJIKITA KUPELEKA WATOTO SHULE ZA VIPAJI!

  Na. Makundi DJ

Shule ya Msingi Chidachi iliyoko katika Kata ya Mkonze Manispaa ya Dodoma; imefanikiwa kufaulisha wanafunzi wote waliohitimu darasa la saba 2011. Shule hiyo iliyoanzishwa mwaka 2004 ilifanikiwa na imeendelea kuwa na mafanikio makubwa kitaaluma tangu mwaka 2006 ambapo wanafunzi wake wamekuwa wakifaulu kwa kati ya asilimia 86% hadi 100%.

Kwa mujibu wa taarifa ziliziopatikana katika shule hiyo; uongozi wa shule sasa unajikita kuongeza uwezo wa watoto kitaaluma ili wafaulu kwa kiwango cha jiuu na kuchaguliwa kwenda kwenye shule a watoto wenye vipaji maalum.

Licha ya mafanikio ya Chidachi inakabiliwa na changamoto kubwa ya uhaba wa vitabu, madawati, vyumba vya madarasa na vifaa vya micheo pamoja na viwanja vya michezo kwa wanafunzi hao.

Uongozi wa shule hiyo hivi sasa pamoja na mikakati hiyo unatafuta wafadhili na wadau mbalimbali kwa lengo la kuchangia maendeleo ya shule ya shule hiyo katika taaluma na michezo.

Shule ya Chidachi ni miongoni mwa shule mpya zilizojengwa katika program ya awali ya Mpango wa Maendeleo ya Elimu ya Msingi (MMEM).

___________________________________________________________________________

CHAVITA YALIA NA KUSAHAULIWA NA SERIKALI.             Na. Barakaelly Mosi

Chama cha Viziwi Tanzania (CHAVITA) kimesikitishwa na kitendo cha Serikali kuwasahau katika mipango yake na kuwafanya walemavu kuwa omba-omba kutokana na kusahauliwa huko. Hayo yalielezwa na washiriki wa mjadala wa kuangalia changamoto za walemavu wasiosikia (Viziwi) lililoandaliwa na CHAVITA kwa ufadhili wa Jumuia ya Kiraia ya The Foundation for Civil Society.

Washiriki wa mjadala huo walisikitishwa na kitendo cha serikali kushindwa kuajiri wataalam wa lugha ya alama katika taasisi zake muhimu kama Polisi, Mahakamani, Bungeni, Hosipitali, ofisi za Halmashauri na Televisheni ya Taifa ili kurahisisha uwasilishaji wa taarifa kwa walemavu hao bila sababu zozote za msingi. 

Washiriki hao walisema kuwa serikali haina nia ya dhati ya kuwapatia wenye ulemavu wa kusikia haki yao ya msingi ya kuwapatia taarifa kutokana na kuwa wataalam wa lugha ya alama wapo; taasisi zake zinazo fedha za kuweza kuwaajiri lakini hawafanyi hivyo, tatizo ni nini? walihoji.

Aidha walieleza kuwa chama chao kiko tayari kutoa mafunzo kwa watu mbalimbali wenye nia ya kujifunza lugha ya alama ili waweze kurahisisha mawasiliano baina yao miongoni mwa jamii. walitoa rai kwa mashirika, taasisi na vyama mbalimbali vya kiraia kuwa na utaratibu wa kujifunza luhga ya alama ambayo walidai ni rahisi kujifunza na kueleweka kwa urahisi.

******************************************

MARAFIKI WA ELIMU WAJADILI MSWADA WA SHERIA YA UZAZI SALAMA

Na. Davis. Makundi

Wanaharakati wa Elimu kupitia asasi ya Marafiki wa Elimu Dodoma wamepata fursa ya kuijadili rasimu ya Mswada wa sheria ya uzazi salama 2012; na kutoa maoni yao juu ya namna ya kuuboresha mswada huo ambao baadaye utakuwa sheria kamili baada ya kupitishwa na Bunge na kusainiwa na Mh. Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Wawakilishi wa Club za marafiki wa Elimu kutoka katika shule za Sekondari za Kikuyu ambayo ni ya serikali na shule binafsi ya Jamhuri zote kutoka Manispaa ya Dodoma; walionesha ushiriki wa hali ya juu katika kuchangia mawazo juu ya mswada huo uliofanyika katika ukumbi wa CCT mjini Dodoma.

Mjadala huo ulioandaliwa kwa ushirikiano baina ya mashirika ya CARE International, Chama cha Wanasheria Wanawake Tanzania (TAWLA) na Shirika la Utepe Mweupe ambapo Mkoani Dodoma mwenyeji wa mashirika hayo ilikuwa asasi ya Marafiki wa Elimu Dodoma (MED).

Washiriki hao walipendekeza kuwa katika mtaala wa elimu liwepo somo la Afya ya Uzazi kwa wanafunzi wa kuanzia angalau darasa la tano na kuendelea hadi katika vyuo ili kuifanya jamii ipate uelewa wa kutosha kuhusiana na suala la uzazi wa mpango na manufaa yake katika jamii na taifa.

Ili kuepuka suala la ndoa za utotoni ambalo licha ya kuwa sasa linapigwa vita na watu mbalimbali huku sheria ikitoa mwanya wa uwepo wa ndoa hizo; washiriki hao walipendekeza muda wa kufunga ndoa uwe angalau miaka 21 muda mambao kwa mtoto wa kike atakuwa angalau amehitimu elimu ya sekondari. 

Majadiliano hayo pia yaliambatana na maswali na majibu kutoka pande zote zilizoshiriki (Wawezeshaji na wanafunzi) ambapo kila upande ulionesha umahiri mkubwa katika kuuliza na kujibu maswali hayo. Katika mjadala huo maswali kuhusiana na sheria ya makosa ya kujamiiana 1999 na maswali yahusianayo na Afya ya uzazi yaliulizwa kwa wingi hali iliyoufanya mjadala huo kutoa nafasi kwa idadi kubwa ya washiriki kuchangia.

Washiriki waliomba serikali, taasisi mbalimbali na asasi zisizo za kiserikali kuwezesha kufanyika kwa mijadala ya aina hiyo mara kwa mara ili kukuza uelewa wa wanafunzi na Club za marafiki wa Elimu ili elimu hiyo iyafikie makundi mbalimbali ya jamii kwa haraka.

Akifunga mjadala huo Meneja wa Miradi kutoka sherika la CARE International Bw. David Lyimo aliwataka washiriki kuimarisha Club zao na kuongea bidii katika masomo ili kuwa mfano katika jamii ndani na nje ya shule kwa kufanya vyema kila wakati katika masomo yao pamoja na tabia zao kwa ujumla.

MCHAKATO WA KUPATA WAJUMBE WA BODI YA MED WAANZA.  Na. Bentez Fares.

Asasi ya Marafiki wa Elimu Dodoma (MED) imeanza mchakato wa kutafuta Wajumbe wa Bodi yake kwa ajli ya kusimamia shughuli za Asasi hiyo. Mchakato huu umeanza siku chache baada ya MED kuwasilisha Katiba na vielelezo muhimu kwenye Ofisi ya Msajili wa Asasi za Kiraia katika Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia na Watoto na kuahidikwa kupata hati ya usajili ifikapo Ijumaa ya tarehe 10 Februari; 2012.

Katiba ya MED inaelekeza kuwa kutakuwa na Bodi ya Ushauri ya MED ambayo itasimamia Sekretarieti ya MED katika utekelezaji wa wa majukumu na kuwasilisha taarifa yake kwenye Mkutano Mkuu wa Wanachama.

Bodi ya MED itakutana mara nne kwa mwaka katika vikao vyake vya kawaida na pia inaweza kuitisha mkutano wa Bodi wa dharura wakati wowote itakapoonekana inafaa kufanya hivyo.

Ili kuwepo na uwiano wa kijinsia katika Bodi hiyo; Katiba ya MED inaelekeza kuwa wajumbe watakuwa tisa na kati yao lazimama watatu kati yao wawe wanawake. Kwa mujibu wa katiba hiyo; wanawake wanaweza kuchaguliwa kwa idadi yoyote kuingia kwenye Bodi hiyo.

Kwa mujibu wa taarifa za ndani ya MED wajumbe wa Bodi wanapaswa kuomba kupata nafasi hizo. Asasi ya MED ni miongoni mwa asasi chache za Mkoa wa Dodoma zinazo juihusisha na Elimu, Demokrasia, Utawala Bora na utetezi wa Haki za Wanafunzi.

MED Yaanza Mchakato wa kupata Usajili wa Kudumu. (Na Prince Kimaro)

Asasi ya Marafiki wa Elimu Dodoma (MED) imeingia katika mchakato wa kupata usajili wa NGO ili kuongeza ufanisi katika kazi zake baada ya kufanya kazi kama CBO kwa kipindi cha miaka mitatu.

Mratibu wa MED na mwanaharakati wa Elimu na Maendeleo Mkoani Dodoma Bw. Davis Makundi amesema ana uhakika kwa kazi zilizofanywa na MED katika hatua ya CBO; zinatosheleza sasa kujikita katika hatua ya juu zaidi ya kuwa NGO ili kufanya kazi katika eneo kubwa zaidi Mkoani Dodoma.

Bw.  Makundi pichani alieleza kuwa anajua kuwa eneo alilochagua ni gumu na lina changamoto nyingi ambazo zitahitaji umakini katika kuzikabili na kufikia malengo ya uwepo wa asasi hii. "Sekta ya Elimu; suala la Demokrasia; changamoto ya Utawala bora na haki za makundi mbalimbali wakiwemo vijana hasa wanafunzi, wanawake, wenye changamoto za ulemavu nk tutazifanyia kazi kwa umakini mkubwa ili kurejesha faraja kwa makundi hayo.

Bwana Makundi amesema MED itasajiliwa kama NGO itakayo fanya kazi zake katika Mkoa wa Dodoma na kujihusisha na uhamasishaji katika kuboresha Elimu, Demokrasia, Utawala Bora, haki za wanafunzi, kuimarisha mawasiliano baina ya jamii na serikali pamoja na  kupambana na umaskini miongoni mwa jamii. "Kufanya kazi kwenye NGO ni kutumikia umma; ni lazima tujitoe na kuweka rehani maisha yetu kwa ajili ya Taifa" Alisema.

Akizungumzia suala la mchakato wa Katiba mpya ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Makundi amesema suala la Katiba ni la watanzania wote bila kujali kiwango chao cha Elimu, taaluma, umri, hali ya kifedha na hata kiafya; hivyo mjadala wa katiba uwe huru na kila mtu apate nafasi ya kutoa maoni yake bila kuwepo kwa kipingamizi.

Asasi ya MED imekuwa ikiendesha mijadala, mikutano ya majadiliano, kuanzisha Club za Marafiki wa Elimu katika shule za Msingi na sekondari ambazo zimekuwa zikijadili masuala mbalimbali yanayo wakabili wanafunzi katika shule zao.

Shughuli za Marafiki wa Elimu Dodoma zimeongeza chachu ya harakati katika maeneo mengi ya mji wa Dodoma hasa kwa wanafunzi wa shule za msingi na sekondari ambao hivi sasa wanaendesha club zao kutetea haki za wanafunzi, maendeleo ya shule, masuala ya demokrasia, utawala bora na maendeleo ya jamii katika maeneo yao.


large.jpg

Kazi ya kufuatiliaa taarifa za Changamoto za Elimu kwa Wanafunzi wa shle ya Kata ya Mbabala Sekondari Manispaa ya Dodoma.

large.jpg

Katika Bunge hili la Tano; Mswada wa kujadili kuanzishwa kwa Katiba Mpya ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania utajadiliwa. Usikose kuwasilisha mawazo yako; KATIBU SANA.