Envaya
Uru rupapuro ruragaragazwa mu rurimi rw'umwimerere Icyongereza. Edit translations

Relaxer na Afya ya Msichana/Mwanamke.

Relaxer ni dawa ya nywele inayofanya nywele za mtu mwenye ngozi nyeusi wa asili ya Afrika zilainike na kunyooka kama nywele za wazungu. Watu wengi hasa wanawake wanapenda kutumia relaxer ili nywele zao ziwe na mwonekano tofauti. Kihistoria matumizi ya relaxer yalianza kama matokeo ya watu weusi kubaguliwa. Watu weusi walipoona hivyo waliamua kuiga maisha ya kizungu ili kufanana fanana na wazungu kwa rangi ya ngozi na nywele ili wathaminiwe na kupewa upendeleo wa kupata fursa za mafanikio na watawala wetu enzi za ukoloni. Wakoloni waliwapendelea watu walioipokea kasumba hii kwa mikono miwili.

Siyo lengo langu kuingia kwa undani katika historia, ila ninajaribu kukupa picha ya chimbuko la matumizi ya kitumwa ya dawa zinazodhuru afya ya watu weusi kwa kiwango kikubwa. Pia kupitia mada hii najaribu kukupa uelewa ili unapofanya uchaguzi wa kutumia au kuacha, uchaguzi wako ujengwe katika uelewa sahihi na siyo katika mkumbo au msukumo wa kijamii unaowaona watu wasiotumia dawa hizi kama washamba.

Sayansi inaonyesha kuwa matumizi ya relaxer za nywele yanaweza kusababisha au kuongeza hatari ya kupata magonjwa ya moyo, kupungua kwa uwezo wa kiakili katika kufikiri na kupambanua mambo, kuungua kwa ngozi ya kichwa na muwasho wa ngozi. Matatizo mengine ni saratani ya matiti, mabonge katika mji wa mimba (Leiomyomata), upungufu wa kinga ya mwili na kubalehe mapema kwa wasichana. Katika utafiti uliofanywa na wanasayansi Lauren A. Wise na wenzake (Wise et al, 2012) na kuchapishwa katika jarida la American Journal of Epidemiology ilibainika kuwa matumizi ya relaxer yanaongeza hatari ya kupata mabonge katika mfuko wa kizazi.

Mabonge yanaweza kusababisha ugumba hasa pale yanapokuwa makubwa na kulazimisha tiba ya upasuaji ya kuondoa kizazi (hysterectomy). Katika jamii za wanawake wanaotumia relaxer kwa kiwango kikubwa, chanzo kikubwa cha upasuaji wa kuondoa mfuko wa uzazi ni mabonge. Inasemekana kuwa katika nchi ya Marekani wanawake weusi wanakabiliwa na tatizo la mabonge mara mbili hadi mara tatu zaidi ya wanawake wengine. Hii inaweza kuwa na uhusiano wa moja kwa moja na matumizi makubwa ya vipodozi kama relaxer.

Hapa Tanzania utafiti unaonyesha kuwa takribani asilimia 10 ya wasichana na wanawake waliokatika umri wa kuzaa wanakabiliwa na tatizo la Mabonge katika mji wa mimba (Kabala, 2011). Hali ya namna hii pia imeonekana katika utafiti uliofanyika nchini Naigeria, nchi yenye watumiaji wengi wa relaxer katika Afrika (Obiechina et al, 2009)

Viambato vilivyomo ndani ya dawa hii hupenya na kuingia katika mfumo wa damu na kwenda kuvuruga mfumo wa vichocheo vya ujinsia hasa homoni za kike. Relaxer nyingi za nywele zina kiwango kikubwa cha kemikali kama vile lye (Sodium hydroxide au Caustic soda), calcium hydroxide, guanidine carbonate, thioglycolic acid salts na monobutyl phthalate.

Rejea

  • Majani, C.B (2013): Afya na Urembo wa Msichana;Lulu publishers.
  • Kabala, R.B (2011): Imaging Finding in Infertile Patients who underwent Hysterosalpingoraphy Investigation at Muhimbili National Hospital, Master’s Thesis (MUHAS). Accessed at http://ihi.eprint.org/id/eprint/935
  • Obiechina et al (2009):Clinical Pattern and Management Outcome of Uterine Fidroids seen in a Private Specialist Hospital in Southeast Nigeria. Tropical J. of Medical Research, vol 13(1),2009.
  • Wise et al (2012): Hair Relaxer Use and Risk of Uterine Leiomyomata in African-American Women, American Journal of Epidemiology (2012) vol. 175(5):432-440.

Kwa habari zaidi bofya na usome hapa: Dawa za nywele zinazosababisha uvimbe wa kizazi kwa wanawake

29 Ukuboza, 2013
« Inyuma Ahakurikira »

Tanga igitekerezo

Izina ryawe:
Aho uherereye
Your email:
(optional)
Your email address will not be published.