Envaya

Tafsiri: English (en): Maandiko ya Watumiaji: WI00053F527069B000010239:content

Asili (Kiingereza) English

 

Mwanza Education & Talent Integration Initiatives (METI)

P. O.Box 10288. Mwanza

Utangulizi. 

Asasi yetu inaitwa Mwanza Education And Talent Integration Initiatives (METI). Ni asasi isiyo ya kiserikali (AZAKI), makao yake makuu yakiwa jijini Mwanza katika jengo la CCM kata ya Buhongwa wilaya ya Nyamagana. Asasi hii ilianzishwa mwaka na wanachama kumi 2008 na kupata usajili rasmi wa kitaifa mwezi Juni 2009 kwa namba 00NGO/0003213. Kwa sasa inafanya kazi katika wilaya za Nyamagana na Ilemela zinazounda halmashauri ya jiji la Mwanza.

Lengo la asasi ni kuibua, kukuza na kuendeleza vipaji vya watoto wanaoishi katika mazingira hatarishi ili kuwajengea uwezo wa kudumu na kuendeleza maisha yao badala ya kuendelea kuwa mzigo na kero kwa jamii. Walengwa wakuu wa asasi hii ni watoto wanaoishi mitaani na watoto wanaoishi katika familia maskini sana wakiwemo yatima waliofiwa na mzazi mmoja au wote ambao walikuwa tegemeo la maisha yao.

Madhumuni ya METI:

  1. Kutoa elimu ya Stadi za Maisha kuwawezesha watoto/vijana kujiepusha na tabia hatarishi (ngono holela, matumizi ya dawa za kulevya, ulevi, nk) zinazowasababisha kuambukizwa magonjwa ya ngono pamoja na Virusi vya UKIMWI

Malengo ya Muda Mrefu ya Asasi: 

  1. Kupunguza idadi ya watoto wa mitaani ambao wameanza kuwa tishio kwa ustawi na usalama wa jiji letu na taifa kwa ujumla
  2. Kubadili maisha ya watoto wanaoishi katika mazingira magumu hasa wale wa mitaani kwa kuinua vipaji vyao ili wawe nguvu kazi ya jamii wanamoishi na Taifa kwa ujumla.
  3. Kuwajengea uwezo watoto wanaoishi katika mazingira magumu (mfano wale wa mitaani) kwa kuwafundisha stadi za kazi zitakazowasaidia kujitegemea. (Kuwapa ujuzi, mbinu na stadi za kumudu na kuendeleza maisha yao)

 Ufafanuzi wa nembo ya asasi

 

 Nembo ya asasi ina vitu vifuatavyo:

  1. Seti ya vifaa vya michezo - kiwakilishi cha Elimu kwa michezo
  2. Brashi- kiwakilishi cha Sanaa za ufundi
  3. Alama ya muziki - kiwakilishi cha Sanaa za muziki    
  4. Ngoma- kiwakilishi cha sanaa za maonyesho
  5. Taa ya umeme – kiwakilishi cha nuru kuwaangazia watoto waishio katika mazingira magumu
  6. Kitabu – kiwakilishi cha Elimu rasmi (ya msingi) 

WANACHAMA WA METI

Uanachama katika asasi ya METI ni wa hiari na unategemea mtu kukubaliana na katiba ambayo inaongoza asasi. Kila anayejiunga na asasi hutoa kiingilio kilichokubaliwa pamoja na ada ya kila mwezi. Kwa sasa asasi ina wanachama 15 wote wakiwa ni waajiriwa katika serikali kuu, serikali za mitaa pamoja na mashirika ya umma. Wachache ni wajasiria mali wenye kujiajiri. Kiingilio na ada za wanachama ndiyo chanzo kikuu cha asasi kwa ajili ya matumizi muhimu ya asasi kama vile kulipia pango, samani za ofisi pamoja na vifaa vya ofisi. Bado asasi haijapata ruzuku toka kwa wafadhili na juhudi zinaendelea kuwatafuta wahisani watakaosaidia kufikia malengo yetu. Kwa sasa Foundation for Civil Society Tanzania wameahidi kutoa ruzuku kwa ajili ya kuendesha mafunzo ya ujengaji uwezo wa asasi. Hii itakuwa ni ruzuku ya kwanza kwa asasi na tunaamini itasaidia kufungua milango ya kupata ruzuku kutoka wahisani mbalimbali.

SHUGHULI ZA METI 

Hivi sasa asasi imekwishafanya utafiti katika kata saba za jiji la Mwanza (wilaya za Nyamagana na Ilemele) kwa ajili ya kuwabaini watoto wanaoishi katika mazingira hatarishi. Lengo ni kubaini sababu za mazingira magumu wanamoishi na madhila ya maisha yanayowakabili pamoja na kujua mahitaji yao makuu ya msingi. Utafiti huu umefanyika kupitia shule za msingi na mitaa teule katika kata hizo. Tunaendelea na uchambuzi yakinifu ili baadaye tuone raslimali gani zitahitajika katika kuwahudumia watoto hao. Aidha, asasi imeshaandaa dodoso kwa ajili ya kuwabaini watoto wanaoishi katika mitaa jijini Mwanza ili kupata taarifa za msingi katika juhudi za kutaka kufanya kazi na serikali za mitaa kuwahudumia watoto hawa kwa mujibu wa malengo yetu. 

Aidha, asasi imeshapata eneo ambalo litatumika kujenga kituo cha kutoa huduma tarajiwa kwa watoto waishio katika mazingira magumu. Eneo hili lina eka takriban kumi katika eneo la Kishili katika kata ya Igoma. Pindi tupatapo fedha shughuli za asasi zitahamishiwa katika eneo hili.

VIKAO:

METI inafanya vikao vyake kila mwezi mara moja ambapo wanachama wote huhudhuria ili kujadili masuala ya msingi ya asasi yetu. Tumepanga ratiba ya vikao na kila mwanachama hupaswa kuhudhuria isipokuwa pale anapokuwa na udhuru

  

 Baadhi ya wanachama baada ya kikao cho cha kawaida 

Mawasiliano na asasi yapitie kwa Katibu Mtendaji wa METI – kwa sasa ni Mr. Mafuru Maregesi Yango (contact person) kwa njia zifuatazo:

Email: metimwanza10@gmail.com au myango55@gmail.com

SLP 10288, Mwanza – Tanzania

Simu ya mkononi: (+255) 754 845 084 / 713 340 200 / 732 375 144

 

KARIBU JIJI LA MWANZA (The ROCK city)

 

(Bila tafsiri)

Ili kuhariri tafsiri, lazima ufungue. Fungua · Jiandikishe