Log in
PANGANI COAST CULTURAL TOURISM PROGRAMME

PANGANI COAST CULTURAL TOURISM PROGRAMME

PANGANI, Tanzania

TTB HABARI

BI DEVOTA MDACHI ATEULIWA MKURUGENZI MWENDESHAJI TTB

Bi Devota Mdachi

Na: Ripota wetu

Hatimaye Bodi ya Utalii Tanzania imepata Mkurugenzi Mwendeshaji baada ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kumteua kuanzia tarehe 23 Oktoba, 2015 aliyekuwa akikaimu nafasi hiyo Bibi Devota Mdachi kushikilia wadhifa huo wa juu kabisa katika Bodi hiyo.

Bi Devota Mdachi ambaye pia alikuwa Mkurugenzi wa Masoko wa TTB amekuwa akikaimu nafasi hiyo ya Mkurugenzi Mwendeshaji kwa miaka miwili kabla ya kuteuliwa kuwa Mkurugenzi Mwendeshaji anakuwa mwanamke wa kwanza nchini kushikilia wadhifa huo katika Bodi ya Utalii toka ilipoanzishwa mwaka 1993.

Bi Devota Mdachi aliajiriwa na Bodi ya Utalii Tanzania kama Afisa Habari za Utalii katika tawi la Arusha mwaka 1994 kabla ya kuhamishiwa Dar es salaam mwaka 1998. Mwaka 2000 alipandishwa cheo na kuwa Afisa Habari za Utalii Mwandamizi na baadae Afisa Habari za Utalii Mkuu mwaka 2004 kabla ya kuteuliwa kuwa Afisa Masoko Mkuu mwaka 2010.

Mwaka 2011 Bi Mdachi alifanyakazi katika Idara ya Masoko na Mawasiliano ya Shirikisho la Utalii la nchi

za kusini mwa Afrika – RETOSA nchini Afrika Kusini

kwa muda miezi mitatu kabla ya kurejea mwaka June, 2011 na kuteuliwa kuwa Mkurugenzi wa Masoko mwaka 2014.

Mdachi ambaye pia ni miongoni mwa wanawake watano wa Tanzania walioshinda tuzo ya wanawake ya Mwl Nyerere (Mwl Nyerere Golden Award Women Achievers) ya mwaka 2015, ana shahada ya kwanza ya Uhusiano wa Kimataifa na lugha ya Kifaransa kutoka Chuo Kikuu cha Dar es salaam. Aidha ana shahada ya Uzamili katika Utalii Chuo Kikuu Huria cha Tanzania na Post graduate certificate ya Utalii kutoka shule ya Kimataifa ya Utalii iliyoko Rome Italia.

 

SAMATA KUWA BALOZI WA UTALII WA TANZANIA?

Na: Ripota wetu

Mwanasoka bora wa Afrika kwa wachezaji wa ndani ya Afrika Mbwana Samata huenda akatunukiwa heshima ya kuwa balozi wa heshima wa Tanzania endapo mazungumzo yanayoendelea baina ya TTB na mawakala wa mchezaji huyo yatazaa matunda.

Bodi ya Utalii Tanzania imedhamiria kumtumia mchezaji huyo katika kuitangaza Tanzania kama eneo la utalii pamoja na vivutio vyake vya Utalii duniani kwa lengo la kuvutia watalii zaidi nchini.

“Tumeanza mazungumzo na mawakala wa mchezaji huyo ingawa bado hatujafikia muafaka, wenzetu upande wa pili wameomba tuwape muda zaidi wakatafakari zaidi” alidokeza Bw. Geofrey Tengeneza. Alisema mawakala wa Samata walikuja katika meza ya mazungumzo wakiwa na mtazamo wa Kibiashara zaidi wakati sisi tunalenga katika mtazamo wa kutanguliza uzalendo badala ya biashara.

Endapo pande hizo mbili zitaafikiana Mbwana Samata ataungana na mabalozi wengine wa heshima ambao

pamoja na mambo mengine husaidia kuutangaza utalii wa Tanzania. Mabalozi hao na nchi zao katika mabano ni pamoja na Dkt Costa Tungaraza (Australia), Bw. Patrick Steenburg (USA), Bw. Macon Dunnugan (USA), Dkt. Philip Imler (USA) na Bibi Flavian Matata (USA).

Mbwana Samata ni mchezaji wa kwanza kutoka Tanzania ambaye hivi karibuni alifanikiwa kuwa mfungaji bora na mchezaji bora barani Afrka kwa wachezaji wanao cheza ndani ya Afrika.

 

PMU YAIMARIKA ZAIDI

Hongera kitengo cha PMU kupata wafanyakazi wapya. Ndugu.Edrick Jackob na Reuben Lameck karibuni sana kwenye familia ya TTB.

Bw. Reuben Bhokeye

Bw. Edrick Kipanda

Na: Ripota wetu

Kitengo cha manunuzi cha Bodi ya Utalii Tanzania kimeongezewa nguvu zaidi baada ya wafanyakazi wawili kuhamishiwa Bodi ya Utalii kutoka  maeneo mengine ya utumishi serikalini.

Wafanyakazi hao Bw. Edrick Jakob Kipanda ambaye ni Afisa Ugavi darala la kwanza aliyejiunga na TTB akitokea Wizara yana Umwagiliaji. Bw. Kipande ana shahada ya Uzamili katika Manunuzi na Menejimenti ya Ugavi kutoka Chuo Kikuu cha Mzumbe wakati  Bw. Reuben Lameck Bhokeye ambaye ni Afisa Ugavi Mwandamizi amejiunga na TTB akitokea idara yaTaifa ya Takwimu. Bw Reuben ana Stashahada ya juu ya Manunuzi.

“Najisikia raha sana na amani sana moyoni kwa kupata watumishi hawa wawili katika kitengo changu na hii imenipa ari zaidi ya kazi” alisema mkuu wa kitengo hicho Bi Mcharo huku akitabasamu alipoulizwa na ripota wa TTB habari kuhus namna anvyojisjikia kuongezewa nguvu mpya katika kitengo chake.

Kabla ya hapo kitengo hicho kilikuwa na wafanyakazi wawili Maria Hamson na Alice Mcharo ambaye ni mkuu wa kitengo hicho.

 

MBWAMBO NA MSHANA WASTAAFU RASMI KAZI

Na: Ripota wetu

Utumishi wa Umma  wa wafanyakazi wa siku nyingi Bibi Rose Waridi Mbwambo na Bw. Amani Yohane Mshana umefikia kikomo baada ya watumishi hao kustaafu kazi rasmi hivi karibuni.

Bw. Msahana na Bibi Mbwambo ambao walikuwa waajiriwa wa Bodi ya Utalii Tanzania (TTB) wameitumikia Bodi kwa muda mrefu toka ilipokuwa Shirika la Utalii Tanzania (TTC) na hatimaye Bodi ya Utalii Tanzania.

Bi Rose Mbwambo aliyekuwa mkuu wa kituo cha habari za Utalii cha TTB kilichokuwa mtaa wa Samora jijini Dar es salaam aliajiriwa mwaka 1994 kama Afisa Habari za Utalii na kuendelea kupanda mpaka kufukia Afisa Habari za Utalii Mwandamizi (Senior Tourist Information Officer) cheo ambacho amekitumikia mpaka anastaafu tarehe 17/11/2015

Naye Bw. Amani Johane Mshana aliajiriwa na Bodi ya Utalii Tanzania  mwaka 1996 kama dreva na alifanya kazi katika tawi la Arusha ambako aliendelea kupanda cheo na kufikia ngazi ya dreva Mwandamizi nafasi ambayo amehudumu kuhudumu mpaka alipostaafau rasmi tarehe 31/12/2015.

 

TTB YAIBUKA MSHINDI WA TATU KATIKA BODI BORA ZA UTALII AFRIKA

Na: Ripota wetu

Bodi ya Utalii Tanzania imeibuka mshindi wa tatu miongoni mwa Bodi za utalii bora barani Afrika katika shindano lililoendeshwa na tasisi ya Kimarekani iitwayo Travvy (Travvy Awards) na kutunukiwa tuzo ya bronze.

Bodi ya Utalii ilikuwa miongoni mwa nchi tatu zilizoingia fainali katika kundi la Bara la Afrika. Bodi nyingine mbili zilizoingia katika nafasi bora tatu ni za Afrika ya Kusini na Namibia  ambapo Afrika ya kusini iliibuka mshindi wa kwanza ikifuatiwa na Namibia.

Akizungumzia ushindi huo Mkurugenzi Mwendeshaji wa Bodi ya Utalii Tanzania Bi Devota Mdachi alisema ushindi huu unaonyesha jinsi gani tunajituma na kufanya kazi kwa weledi licha ya changamoto kadhaa zinazotukabili. “Ushindi huu ni kielelezo kwamba tunafanya kazi nzuri pamoja na changamoto kadhaa tulizo nazo” alisema Bi Devota. Aliongeza kuwa nafasi ya tatu tuliyoipata imetupa faraja na kututia hamasa sana na huu ni ushindi wa nchi na wadau wote wa sekta ya utalii kwa ujumla.

Bi. Devota Mdachi

Bi. Devota Mdachi - Mkurugenzi Mwendeshaji-Bodi ya Utalii Tanzania.

TTB YAPOKEA WANAFUNZI KWA AJILI YA MAFUNZO KWA VITENDO

Na: Ripota wetu

Wanafunzi kutoka vyuo mbalimbali hapa nchini wameendelea kupata nafasi ya kujifunza kwa vitendo (practical) Bodi ya Utalii Tanzania katika idara na vitengo mbalimbali baada ya kupata mafunzo yao kwa njia ya ndaharia wawapo vyuoni.

Hivi karibuni TTB imepokea wanafunzi wawili Happy Boniface Choma wa mwaka wa kwanza katika Chuo cha Taifa cha Usafirishaji (NIT) anayesoma kozi ya Menejimenti ya Raslimali watu (Human Resoursce Management). Bi Happy Choma ambaye yuko katika idara ya Utawala na Raslimali watu atakuwa TTB kwa mafunzo mpaka mwezi Machi 2016.

Mwanafunzi mwingine ni Happy Mchekelo Lenis wa Chuo cha VETA Mtwara anayesomea Ukatibu Muhutasi naye atakuwa hapa mpaka Machi 2016 akiwa chini ya Bi Hidaya Kayera.

Bodi ya Utalii imekuwa na utaratibu wa kutoa fursa kwa wanafunzi kutoka vyuo mbalimbali hapa nchini kujifunza kwa vitendo kozi wanazosomea katika vyuo wanavyotoka.

Bi Happy Choma

Bi. Happy Mchekelo

WAWILI WAAJIRIWA TTB KWA MKATABA WA MUDA

Na: Ripota wetu

Katika kuimarisha utendaji wake na kuboresha wa huduma izitoazo kwa wadau mbalimbali wa ndani ya shirika na nje, Bodi ya Utalii Tanzania imeajiri vijana wawili kwa mkataba wa mwaka mmoja mmoja kila mtu.

Watumishi hao ambao wako katika ajira ya muda toka tarehe 09/11/2015 wote wanahudumu upande wamapokezi (reception) na kabla ya kujiunga na TTB walikuwa katika maeneo mengine ya utumishi na chuoni.

Bi Zainab Lugwani ambaye ana cheti cha Front office operation kutoka chuo cha Taifa cha Utalii (National college of Tourism) amejiunga na TTB akitokea katika hotel ya Blue pearl iliyopo ubungo ambako pia alikuwa upande wa mapokezi. Nae Bi Husna Mohammed amejiunga na TTB akitokea masomoni chuo cha Taifa cha Utalii ambako alihitimu stashahada ya Front office operation. Kabla ya hapo Bi Husna alifanya kazi Msalaba Mwekundu (Red Cross Tanzania) akiwa ni mtunza stoo (store keeper).

Waajiriwa wapya Bi Zainab Lugwani (kushoto) na Bi Husna Mohammed

 

BODI YA UTALII TANZANIA YAWANIA TUZO YA MWAKA YA KIMATAIFA YA WORLD TRAVEL AWARDS

Na: Ripota wetu

Bodi ya Utalii Tanzania ni miongoni mwa taasisi na vivutio 24 vya utalii vya Tanzania vulivyoingizwa kwa ajili ya kuwapata washindi wa Annual World Travel Awards (AWT) kwa makundi (categories) mbalimbali katika sherehe ya utoaji tuzo hizo ambazo mwaka huu zitafanyika April 9 mwaka huu  Zanzibar katika hotel ya Diamonds La Gemma dell’Est

Bodi na Mamlaka nyingine za Utalii zinazoshindanishwa na TTB katika chini ya Destination category katika kundi la Bodi zinazoongoza Africa kwa mwaka 2016 ni pamoja na Mamlaka ya Utalii ya Misri, Bodi ya Utalii ya Gambia, Mamlaka ya Utalii ya Ghana, Bodiya Utalii ya Kenya, na Shirika la Taifa la Utalii la Morocco. Mengine ni Bodi ya Utalii ya Namibia, Shirika la Maendeleo ya Utalii la Nigeria na Kamisheni ya Utalii ya Zanzibar.

Taasisi nyingine na vivutio vya utalii kutoka Tanzania vilivyoingizwa kuwania tuzo hizo na makundi yao katika mabano ni Uwanja wa ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere Julius Nyerere, Bandari za Dar es salaam na Zanzibar, Zanzibar kama eneo la utalii, Mlima Kilimanjaro, Bonde la Ngorongoro, na  Hifadhi ya Taifa ya Serengeti.

Nyingine ni hotel ya Diamond La Gemma dell’Est, Hoteli ya Dream of Zanzibar na Hideaway of Nungwi Resort &Spa, Hoteli za Blue bay Beach Resort & , Dream of Zanzibar, Karafuu Beach Resort &Spa na Diamond La Gemma dell’Est zote za Zanzibar: Serena Hotel –Dar es salaam; Singita Sasakwa Lodge; Breezes Beach Club na Karafuu Beach & Spa; Beyond Mnembe Island Lodge na Chapwani Private Island: Four Season Safari Lodge Serengeti; Singita Sabora Camp na Jongomero Camp.

Upigaji kura umeanza Februari Mosi mwaka huu na umefikia mwisho Februari 29, 2016.

 

Imetolewa Na:

BW. GEOFREY TENGENEZA

Mhariri Mkuu TTB HABARI.

Simu: +255222127424

Mobile: +255 713 439 928

Email: gtengeneza@tanzaniatourism.go.tz

 

Tuandikie:

 

BODI YA UTALII TANZANIA

Utalii House — Mtaa wa Laibon / Barabara ya Ali Hassan Mwinyi, Karibu na ubalozi wa Ufaransa

S.L.P 2485

Dar es Salaam, Tanzania

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

« Previous Next »

Add a comment

Your name:
Your location:
Your email:
(optional)
Your email address will not be published.